Thursday, March 20, 2014

FAHAMU MAAJAMU YA KITUNGUU SWAUMU KWA AFYA YAKO



KITUNGUU SAUMU MKOMBOZI WA UCHUMI NA AFYA
Kitunguu swaumu (Garllic) ni zao lenye manufaa sana kiafya na katika kuinua kipato cha mkulima. Ulimaji wake hauna gharama kubwa endapo litalimwa kwa kuzingatia wakati  na eneo stahiki.

Zao hili ni miongoni mwa viungo muhimu vya chakula hapa nchini na vinavyotumika kwa wingi. Aidha, zao hili limepata umaarufu mkubwa katika kuweka harufu kwenye chakula muhimu sana hapa Tanzania (pilau) na kinachopendwa na wengi katika sikukuu mbalimbali. Ingawa wengi hukitumia kuongeza harufu kwenye chakula hicho bado hawajafahamu manufaa yake kiafya na kiuchumi.
Historia inaonyesha kuwa, vitunguu saumu vilianza kutumika China mwaka 510 K.K na pia vilitumiwa na wanajeshi wa Ugiriki na Roma. Zao hili pia lilianza kutumika katika maabara mbalimbali duniani hususani Asia, Afrika na Ulaya takribani miaka 6000 iliyopita. Matumizi makuu nyakati hizo yakiwa viungo katika mboga na tiba.

Kutokana na viasilia mbalimbali vinavyopatikana katika zao hili na zinazofanya kazi tofauti, zimeisaidia kuwa na uwezo na faida nyingi katika mwili wa binadamu hasa kutumika kama kinga na tiba ya maradhi mbalimbali.

Udongo
Kitunguu saumu huota zaidi ukanda wa juu kuanzia mita 900 hadi 1500. Pia huota katika udongo wa aina yeyote lakini hustawi zaidi katika udongo usiotuamisha maji. Udongo huo ni lazima uwe na mbolea ya kutosha hasa ya asili.

Ikiwa udongo wako ama ardhi unayotumia kuotesha kitunguu chako haina mbolea ya kutosha basi hakikisha unaurutubisha kwa kuweka mboji ama samadi iliyoozeshwa vizuri. Pia waweza kuweka samadi mbichi iliyotoka moja kwa moja zizini katika shamba lako kisha kulilima huku ukichanganya samadi na udongo vizuri na kuliacha kwa muda wa miezi saba hadi kumi kisha kulilima tena na kuotesha vitunguu vyako.

Mbolea za viwandani kama Ammonium Sulphate, Ammonium Nitrate, DAP, Urea na nyingine zaweza kutumika kwa kiwango kitakachoshauriwa na wataalamu wa kilimo na kwa muda sahihi japo hatukushauri sana kuitumia kwani mbolea ya samadi pekee yatosha.

Hali ya hewa
Kwa nchi ya Tanzania, zao hili huoteshwa na kusitawi vizuri katika kipindi ambacho joto ama ni la wastani. Iwe ni kipindi cha baridi japo si baridi sana (Nyuzi joto 18C hadi 22C).


Utayarishaji wa shamba
Hakikisha shamba lako lipo katika eneo zuri lisilotuamisha maji na lisafishe vizuri kwa kuondoa magugu yote na kisha kuyafukia kwani ni rutuba pindi yakioza. Weka mboji na kisha lilime vizuri kwa kuchanganya mbole na udongo tayari kwa kuotesha.

Utayarishaji wa mbegu
Vitunguu vinavyoota vizuri ni vile vilivyohifadhiwa sehemu nzuri isiyokuwa na unyevu, na katika eneo lenye joto la wastani. Kama utahifadhi katika sehemu yenye joto jingi na hakuna hewa ya kutosha basi ukiviotesha vitunguu hivyo vitazalisha mavuno duni na dhaifu.

Kabla ya kupeleka shambani, chukua kitunguu saumu na kuchambua kwa kutenganisha vitunguu kimoja kimoja kisha kuchagua vile vitunguu vikubwa kwa kuwa hivi ndivyo vitakavyokupatia mavuno mengi na vitunguu vyenye ubora, kisha peleka shambani tayari kwa kuotesha.

Namna ya kuotesha
Piga mashimo kama ya kuoteshea maharage. Nafasi kati ya mche na mche iwe ni sentimeta 8-12 na kati ya mstari na mstari iwe ni sentimeta 25-30 (visiwe mbalimbali kama kitunguu maji kwani vitunguu swaumu havinenepi sana na unapootesha karibu ndipo unapokuwa na kiwango kikubwa cha mavuno.

Weka kitunguu chako katika mashimo ukihakikisha kuwa mizizi inakuwa chini na shina linaangalia juu. Hakikisha vitunguu vyako haviegemei upande wowote bali vimesimama wima.
Baada ya kuweka katika mashimo, fukia kwa udongo wa kutosha na uukandamize kwa nguvu kiasi ili kuhakikisha kitunguu chako kimekaa vizuri na hakiwezi kuanguka ama kuathiriwa na kitu chochote kama kung’olewa na mvua au maji wakati wa kumwagilia. Pia kwa kufanya hivyo utakinga mazao yako kuharibiwa na wanyama kama mbwa wakati wakikatisha na hata kuingia katika shamba lako.

Kuchipua
Baada ya siku kumi hadi siku kumi na sita, kitunguu swaumu kitachipua na kuanza kutoa majani hadi kumi na sita. Jani la katikati ambalo litaweka mbegu, litaendelea kukua na kupita majani mengine kwa urefu (mbegu hiyo ni kitunguu na huwa ni kimoja tu, lakini utakapokiotesha baada ya kuvuna kitaota na kuzaa vitunguu vingine vingi).

Umwagiliaji
Kwa kipindi cha mvua, huna haja kabisa kumwagilia kwani maji ya mvua tayari yanatosha. Kama ni kipindi cha kiangazi hakikisah unamwagilia vitunguu vyako kila unapoona shamba limekauka. Unaweza kumwagilia mara mbili hadi tatu kwa wiki.

Usimwagilie vitunguu wakati wa mchana au jioni. Ni vizuri sana kumwagilia wakati wa asubuhi ili kuipa uwezo wa kupambana na magonjwa kwani wakati kama wa jioni utaongeza uwezo wa vitunguu kushambulia na barafu na hata kuoza.

Uwe na utaratibu wa kuchunguza vitunguu vyako kama vimezaliana vya kutosha hasa baada ya miezi miwili kwa kuchimba kidogo. Ukishagundua kuwa vimezaliana vizuri, usimwagilie tena bali viache na kuipa nafasi kukomaa kwani ukiendelea na umwagiliaji basi vitunguu vyako vitaoza.

Usafi wa shamba
Mara zote shamba lako linahitajika kuwa safi kwa kilimo bora. Hakikisha unafanya usafi kwa kung’oa magugu na majani yasiyohitajika ili kuondoa ushindani baina yake na vitunguu vyako ambavyo vitakuwa vikigombea rutuba, hewa na maji.
Ni muhimu sana kufanya palizi walau mara nne hadi tano kufikia mavuno.

Magonjwa
Kama ilivyo kwa mazao mengi ya bustani, kitunguu saumu hushambuliwa na magonjwa kama ukungu, kuoza, fangas pamoja na wadudu.

Namna ya kuondokana na magonjwa hayo
Ni muhimu sana kudhibiti magonjwa haya mara tu uonapo dalili kwa kutumia viuatilifu ili kuondokana na hasara kubwa itakayotokea.

Unatakiwa pia kufanya kilimo cha mzunguko wa mazao katika shamba lako yasiyo jamii moja ya vitunguu saumu kama kuotesha mahindi, maharage ili kuondokana na magonjwa mengine ambayo yanaweza kuwa sugu.

Pia, kuepukana na umwagiliaji wa jioni na usiku pamoja na kuotesha katika maeneo yanayotuamisha maji kutasaidia kuzuia ugonjwa wa kutu kwenye majani na fangas.
Ikiwa mimea tayari imevamiwa na ugonjwa wa kutu, basi mimea yote ing’olewe na kuchomwa ili kuinginga mimea ijayo itakayooteshwa katika shamba hilo.


Kukomaa hadi kuvuna
Kitunguu swaumu huchukua miezi mitatu na nusu hadi minne kukomaa. Utagundua kuwa kitunguu chako kimekomaa na kipo tayari kuvunwa mara baada ya jani lake dogo la mwisho litakapokauka. Hapo watakiwa kuingia shambani na kuvuna.

Namna ya kuhifadhi
Mara baada ya kuving’oa vitunguu vyako, na majani yake yakiwa bado mabichi, chukua kamba na funga mafundo ya ukubwa kiasi (Unafunga kwenye majani), kisha vining’inize juu katika eneo lenye joto la wastani (kusiwe na unyevu wala ubaridi). Vitunguu vyako vitaendelea kukauka taratibu huku vikinyonya yale maji yote yaliyopo kwenye majani yake.

Pia waweza kuvikata majani na kupunguza mizizi baada ya kung’oa kisha kuweka darini na vitaendelea kukauka taratibu.

Kama ulitumia mbolea ya samadi au mboji, waweza kuhifadhi kitunguu chako kwa muda wa miezi saba hadi nane bila kuharibika na ikiwa umetumia mbolea za viwandani basi vitunguu vyako vyaweza kuharibika baada ya miezi mitatu au minne.

Faida za kitunguu saumu kiafya
Kutokana na tafiti mbalimbali zilizofanywa na wanasayansi kama Louis Pasteur, kitunguu swaumu kimegundulika kuwa na uwezo wa kutibu na kukinga magonjwa mengi yanayomsumbua binadamu kila wakati.

Imegundulika kuwa kitunguu saumu husaidia kuzuia maradhi ya saratani pamoja na malaria kutokana na kemikali ambazo hutoka baada ya kukata ama wakati wa kutafuna.

Uchunguzi umebaini kuwa kitunguu saumu huweza kupunguza athari za kemikali nyingine zisizofaa mwilini hasa zitokanazo na moshi na kuimarisha uwezo wa seli za mwili.

Mwaka 1845, mwanasayansi Pasteur aligundua kuwa kitunguu swaumu huweza kutumika kama tiba ya vidonda na huzuia donda ndugu kwa kiasi kikubwa.

Haikuishia hapo, kitunguu saumu pia hutumika kama tiba ya mafua, kuzuia magonjwa ya moyo kwa kupungua kiwango cha lijamu, kupunguza shinikizo la damu na kurekebisha kiwango cha sukari mwilini.
Mwisho


No comments:

Post a Comment